Utafiti wa Maji chini ya Ardhi

Huduma ya utafiti wa kijiofizikia na kihaidrojiolojia unafanywa kwa lengo la kutafuta maji chini ya ardhi, Uchunguzi wa maji chini ya ardhi unapaswa kufanywa kwa kutumia angalau njia mbili za utafiti, mojawapo ni lazima iwe njia ya kusafirisha umeme chini ya ardhi (vertical electrical sounding) mbinu nyingine ni Sumaku-umeme, Nguvu-sumaku, Mvuto, na Mitetemo. Njia inayohusisha usumaku inasaidia kutafuta mikondo ya maji ambayo inapatikana chini ya ardhi, Njia ya pili ni njia ya umeme hii inasaidia kujua umbali wa mikondo ya maji iliyo hai au iliyokufa iliyoko chini ya ardhi. Bodi ya maji ya bonde la Pangani inatoa huduma hii kwa Makampuni, Taasisi za Serikali, Taasisi zisizo za Kiserikali na kwa mtu mmoja mmoja.

Utaratibu wa kupata huduma hii ni

I. Kabla ya kufanya uchunguzi wa maji chini ya ardhi katika eneo lolote, mteja anapaswa kufika Bodi ya Maji  Bonde la Pangani kwa ushauri wa kitaalamu kuhusu eneo analopendekeza kufanyiwa utafiti, Mtu/Kampuni yeyote iliyo na leseni ya uchunguzi wa maji chini ya ardhi, kabla ya kuanza shughuli za uchunguzi wa maji chini ya ardhi, anapaswa kutoa taarifa kwa Bodi ya Maji ya Bonde husika.

II. Mteja ataandika barua ya maombi kwa Bodi ya Maji Bonde la Pangani, na itajibiwa haraka iwezekanavyo na mteja atapewa makadirio ya gharama ya huduma hii na kupewa namba za malipo (control number), na malipo yatafanyika kwa njia ya Kielektroniki.

III. Baada ya mteja kukamilisha malipo wataalamu watafika eneo husika kwa ajili ya kufanya utafiti wa maji chini ya ardhi.

IV. Baada ya utafiti kukamilika mteja atapatiwa ripoti ya utafiti inayoonyesha uwepo au kutokuwepo kwa maji na kina kinachokadiriwa kupatikana kwa maji pamoja na njia itakayotumika katika shughuli ya uchimbaji kulingana na miamba ya eneo husika.